0

Joseph Kapinga  

Fainali za Kombe la Dunia zimekwisha. Ujerumani wametwaa ubingwa wa kuifunga Argentina bao 1-0 katika mchezo wa fainali wiki moja iliyopita nchini Brazil.
Ule mwezi mzima wa mashabiki wa soka kuelekeza masikio na macho nchini Brazil, umepita, hakuna tena stori. Imebaki kumbukumbu na maisha yanaendelea.
Tunarudi nyumbani kwenye soka letu la nyumbani. Soka lenye changamoto za migogoro, majungu, fitina, chuki na visasi.
Ukiona soka limemezwa na mambo hayo, usitarajie hata siku moja mafanikio yakapatikana. Itoshe kusema kwamba, soka letu linahitaji mapinduzi makubwa.
Inasikitisha, siku zinakwenda na hakuna mabadiliko, siyo kwenye klabu wala vyama vya michezo. Migogoro kila kukicha. Yanga wameuongezea uongozi wao muda wa kukaa madarakani. Siyo wote waliopenda uamuzi huo. Hali hiyo tayari inaweza kuzaa mgogoro.
Simba walifanya uchaguzi mkuu hivi karibu. Sote tumeshuhudia yaliyotokea, uchaguzi ulifanyika baada mvutano mkali kiasi cha hata baadhi ya wanachama kwenda mahakamani kutaka kuusimamisha.
Tunamlaumu nani wakati sisi wenyewe ndiyo chanzo cha migogoro? Wenzetu wanalilia kuweka rekodi za mafanikio kwenye mashindano makubwa ya soka, sisi tunapigania kuweka rekodi za kuzalisha migogoro.
Kinachotokea kwenye soka letu, ni sawa na mtu asiyependa kuona watu wanaishi kwa amani, atafanya kila njia kuwagombanisha. Soka letu liko hivyo. Hatuwapi nafasi viongozi, tukiona viongozi wametulia, hakuna migogoro, hakuna chuki, fitina, majungu tunaumia. Tunataka migogoro.
Unajua kwa nini yote haya? Kwa sababu, migogoro kwenye klabu zetu haipendwi, lakini siyo wote wasiyoipenda. Kwenye migogoro, kuna watu wanafaidika nayo. Fikiria, shabiki anayeishi mjini kwa sababu ya kufaidika na migogoro, leo anawezaje kuwa na furaha kama hakuna migogoro? Atakubali vipi kufa njaa wakati ana taaluma ya kulazimisha migogoro kutokea?
Haya ndiyo maisha ya soka letu. Kama vile fainali za Kombe la Dunia zilivyomalizika na maisha yanaendelea kama kawaida, ndivyo hivyo kwetu.
Tumerudi kwenye maisha ya kawaida ya soka letu. Soka ambalo tunatumia muda mwingi kuwekeza migogoro badala ya maendeleo. Alaumiwe nani?
Viongozi wetu wamepitwa na wakati, bado wapofu. Hawana kiu ya maendeleo kupitia kujifunza kwa wenzetu walioachana na uwekezaji kwenye migogoro na kuangalia mbele.
Nchi hii ina vijana wenye vipaji vya hali ya juu. Hatuwaangalii kabisa. Tutaonaje vipaji vyao wakati macho na fikra zetu zimejaa utumwa wa migogoro?.
Tukipenda tunaweza kuleta mageuzi, lakini kamwe hayatapatikana kama tutaendelea kuwa viongozi walewale, wanachama wa migogoro walewale. Tujifunze kutoka kwa wenzetu!

Post a Comment

 
Top