0

 Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu ch Sayansi na Teknolojia (Must), Profesa Joseph Msambichaka  (mwenye miwani katikati) akifuatilia maelezo ya wanafunzi kuhusu utengenezaji wa roboti. Picha na Lauden Mwambona  

Wakati vijana wengi wanaomaliza vyuo mbalimbali wakikosa kazi, wanasayansi katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia (Must)  cha jijini Mbeya kwa kushirikiana na serikali ya Italia, wanatarajia kutoa mafunzo kwa vijana kuhusu utengenezaji wa roboti zinazosaidia kufanya kazi viwandani.
 Mafunzo hayo yataanza Oktoba mwaka huu na yatalenga kutengeneza  roboti zitakazofanya kazi kwenye viwanda mbalimbali vikiwamo vya kutengeneza sukari, nguo, dawa, sabuni  na bidhaa nyingine mbalimbali.
 Makamu Mkuu wa Chuo  hicho, Profesa Joseph Msambichaka  anasema mpango huo wa mafunzo kwa ngazi ya stashahada unatekelezwa kwa ushirikiano na wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Polytechnic of Milan cha Italia.
Anasema  wameanza kwa kuwafundisha wahadhiri 12 kutoka vyuo vitatu nchini, ambao wamefanikiwa kufaulu na kutengeneza roboti moja linaloweza kufanya kazi kwenye kiwanda.
 ‘’Kazi za kisayansi na teknolojia hazihitaji mtu kushika nyundo ili kuzitekeleza, bali zinahitaji utalaamu wa kisasa ukiwamo wa kutumia roboti ili kurahisisha utendaji’’ anasema Profesa Msambichaka.
 Meneja wa mpango huo kwa upande wa Italia kupitia Ubalozi wake uliopo Dar es Salaam, Daniele Cristian Passalacqua anasema  Serikali yake iliamua kuisaidia Tanzania katika masuala ya teknolojia ya matumizi ya roboti  kwa lengo la kuongeza kasi ya maendeleo nchini.
 Anasema Italia kupitia Chuo Kikuu cha Milan itashirikiana na Tanzania kuhakikisha teknolojia hiyo inakuzwa na kufanyiwa kazi kwa lengo la kurahisha kazi na kuongeza ufanisi.
‘’Tayari Serikali yangu inasaidia  elimu ya sayansi kwa wasichana wanaosoma vyuo mbalimbali na hadi sasa wapo wasichana 500 wanaosomeshwa kupitia mpango huu’’ anasema Cristian.
 Anasema mpango wa kufundisha masomo ya kutengeneza roboti utatekelezwa kwenye vyuo vya Sayansi na Teknolojia Mbeya, Chuo cha Teknolojia Dar es Salaam (DIT)  na Chuo cha Ufundi Arusha.
 Ofisa huyo anasema matumizi ya roboti katika masuala ya sayansi na teknolojia nchini, yataiondoa Tanzania kwenye kundi la nchi Masikini zaidi duniani na kuifanya iwe nchi yenye maendeleo.
 Naye Mhadhiri Mwandamizi kutoka Chuo Kikuu cha Polytechnic Of Milan, Profesa Francesco Braghin  ambaye alifika kutoa mafunzo kwa wahadhiri watakaofundisha utengenezaji wa  roboti nchini, anasema  dunia ya tatu  inahitaji roboti ili kuboresha kazi.
 Anasema wanaamini kazi zikifanywa kwa roboti zitafikiwa malengo na uzalishaji utaongezeka kwa vile roboti haina kupoteza muda  wala kufanya uzembe ili mradi uipange vizuri.
Mratibu wa mpango huo katika Chuo Kikuu ch Sayansi na Teknolojia Mbeya, Dk Lusajo Muga  anasema chuo chake kimeupokea kwa moyo mkunjufu mpango huo, baada ya kubaini ukweli kwamba dunia ya leo siyo ya jana.
 Muga ambaye ni mwanamke bingwa katika kitivo cha Uhandisi wa Kompyuta anasema Italia imewasaidia kupata vifaa mbalimbali va maabara na kwamba malengo ni kuwasomesha wasichana wengi  zaidi kutokana na ufadhili kwao unaotolewa na nchi hiyo.
 Anasema Italia imewafadhili wasichana mbalimbali wanaosomea masuala ya sayansi na teknolojia  katika chuo chake , hivyo anawahimiza wasichana  kuongeza bidii ili waweze kufaidi matunda ya msaada huo.
 Anna Kisoki kutoka Chuo cha Teknolojia Dar es Salaam  ambaye ni mmoja wa watakaofundisha roboti nchini, anasema  ana uhakika kwamba wanafunzi watayapenda zaidi masomo hayo kwa vile yatashirikisha zaidi vitendo.
Anasema wanafunzi watajifunza kutengeneza roboti na kuitumia katika kazi za kila siku, jambo ambalo anaamini litaongeza uzalishaji  na ufanisi wa kazi.
‘’Roboti zikitumika kupanga chupa za vinywaji viwandani ama kupanga viroba vya sukari na hata kujaza dawa kwenye chupa, kazi itafanyika kwa urahisi na haraka zaidi’’ anasema Kisoki akieleza faida za matumizi ya roboti maeneo ya kazi.

Post a Comment

 
Top