Wengi hujikuta wakipigwa, wakitukanwa, wakinyanyaswa au wakipewa adhabu kali na walimu wao kutokana na hali zao wakiwa darasani.
Ni maisha ya kawaida tu kwao, japo si hiyari yao
hayo yatokee. Mambo wanayotendewa wanafunzi hawa yamekuwa sugu kiasi cha
kuwafanya wasisome kwa umakini na hatimaye kutengwa na mfumo mzima wa
elimu stahiki.
Hawa ni wanafunzi wenye mahitaji maalumu, wakiwamo walemavu wanaojulikana zaidi katika jamii.
Kimsingi wanafunzi wenye mahitaji maalumu ni kundi
la watoto mbalimbali nchini wakiwamo wale wanatoka kwenye familia duni,
waliotelekezwa, wenye ulemavu wa aina zote, wenye matatizo ya
kisaikolojia na wengineo.
Kundi hili kwa bahati mbaya limejikuta likitengwa
na jamii husika kwa kuwa walimu na wazazi hawajabaini haraka mahitaji
yao ambayo yamekuwa ya nadra sana kusikika au kubainika.
Suala hili ndilo lililowakutanisha wadau
mbalimbali wa elimu hivi karibuni kujadili namna kundi hilo
litakavyosaidiwa ili lipate elimu bora.
Katika mkutano huo ulioandaliwa na Mtandao wa
Elimu Tanzania (TenMet), wadau wanabainisha kuwa watoto wengi wamekuwa
wakihudhuria darasani na kutoka bila ya kuelewa chochote kutokana kukosa
msaada madhubuti kutoka kwa walimu wao.
Hali hii kwa mujibu wa wadau hao inaendelea mpaka
wanapohitimu na kupata alama mbaya na hatimaye kutupwa nje ya jumuiya ya
wasomi.
Uelewa mdogo
Mhadhiri wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu cha Dar
es Salaam, Dk Luka Mkonongwa anasema utamaduni wa kutobaini mahitaji
maalumu ya wanafunzi katika ngazi za chini ndiyo uliofanya watoto wengi
nchini kutengwa.
Elimu jumuishi ni ile inayozingatia mahitaji ya
watoto wote kwa kutoa elimu bora kwa usawa bila kuangalia vigezo vya
uwezo wa kiakili, afya, ulemavu na fedha, anasema na kuongeza:
“Utakuta mwalimu anamwadhibu mwanafunzi
anayesinzia darasani au anampigisha magoti yule ambaye haelewi darasani
bila kufahamu kuwa yule mtoto ana matatizo gani yanayomsumbua. Hilo ni
tatizo la kulitatua haraka.’’
Anasema: “Walimu wengi hawana uelewa juu ya elimu jumuishi.
Hawajafunzwa kabisa, hivyo ni vigumu kuwajali watoto wa aina hii kwa
kuwafundisha katika mazingira rafiki.”
Hoja ya Dk Mkonongwa inaibua mjadala mzito ambao
unang’amua kuwa hata kwenye vyuo vya ualimu elimu jumuishi haifundishwi
ipasavyo na ni taasisi chache zinazotoa kozi zinazofanana na elimu hiyo.
“Ni vyuo vikuu vinne vinavyotoa kozi za elimu
maalumu ambavyo ni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Dodoma,
Chuo Kikuu Huria cha Tanzania na Chuo cha Sebastian Kulowa, Lushoto.
“Hivi vina kozi moja moja tu inayoweza kusaidia
kujenga msingi wa elimu jumuishi wakati Chuo cha Patandi cha Arusha
ndicho pekee kinachofundisha walimu ufundishaji wa watu wenye mahitaji
maalumu,” anasema Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Elimu cha Mkwawa, Daniel
Hyera.
Hyera anabainisha uchache wa vyuo hivyo unaweka
wazi kuwa ni vigumu walimu kufahamu vizuri namna ya kuwalea na
kuwafundisha watoto wenye matatizo mbalimbali.
Pia, wazazi nao hawajafahamishwa aina hii ya elimu kutokana na kukosa fursa ya kupatiwa mafunzo.
Mwalimu Raphael Njiwa wa shule ya sekondari Kaseme
iliyopo mkoani Geita, kwa upande wake anakiri kuwa ni walimu wachache
wanaojitoa kuwasikiliza watoto na kuwafundisha kulingana na mahitaji
yao.
“Kuna wakati unaguswa unamsikiliza mwanafunzi
baada ya kugundua nidhamu au ufanisi wake darasani umeshuka. Wale
wanaokueleza unawapa ushauri na kuwasaidia waweze kuelewa kama wengine,”
anasema Njiwa.
Sera na mitalaa ni tatizo
Hata hivyo, si lawama kwa vyuo pekee kushindwa
kufundisha walimu kuelewa mahitaji maalumu ya wanafunzi, bali hali hiyo
inaikumba pia serikali kwa kushindwa kuandaa mazingira rafiki ya
kuwezesha jitihada hizo.
Serikali inalalamikiwa kushindwa kuandaa sera na mikakati madhubuti ya kutekeleza elimu jumuishi katika ngazi zote.
Pia, utekelezaji wa kususua kwa baadhi ya sera na
mitalaa rafiki kwa elimu bora na inayoleta usawa, unatajwa kuwa chanzo
cha kuwakosesha baadhi ya Watanzania elimu bora.
“Mitalaa mingi imelenga tu katika maudhui badala ya kufanikisha
uweledi na uelewa wa mwanafunzi. Hali hii inawajenga watoto kukariri tu
masomo badala ya kuelewa kinachozungumziwa na hatimaye kuwatenga
wengine,” anasema mtaalamu wa masuala ya elimu, Dk Wilberforce Meena.
Anasema kuwa serikali ina sera nzuri za kuvutia
lakini utekelezaji wake siyo wa kuridhisha kiasi cha kutishia
mustakabali wa elimu.
Post a Comment