0

 
Wiki moja iliyopita, timu ya taifa ya soka, Taifa Stars ilicheza mechi ya kwanza ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza Fainali za Mataifa ya Afrika (CAN 2015) dhidi ya Msumbiji na kutoka sare ya 2-2 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Fainali hizo za 30 za Mataifa ya Afrika zinatarajiwa kufanyika nchini Morocco kuanzia Januari 17 mpaka Februari 8, 2015 na zitashirikisha timu 16.
Mwishoni mwa wiki hii, Taifa Stars itaingia tena uwanjani kucheza mechi ya marudiano na wapinzani hao kwenye Uwanja wa Zimpeto mjini Maputo kuwania kutinga hatua ya makundi kabla ya kupata timu mbili zitakazofuzu kucheza fainali hizo nchini Morocco.
Kama Taifa Stars itaibuka na ushindi katika mechi hiyo, itaingia Kundi F lenye timu za Zambia, Cape Verde na Niger.
Ni wazi baada ya Taifa Stars kutoka sare ya mabao 2-2 na Msumbiji wiki iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam imejiweka katika mazingira magumu ya kusonga mbele.
Hata hivyo, huu siyo wakati wa wachezaji wa Stars, viongozi wa soka, Serikali na mashabiki nchini kukata tamaa kwa sababu ipo mechi ya marudiano mwishoni mwa wiki hii ambayo tunatakiwa kuitumia vema kupata ushindi ingawa tutakuwa ugenini.
Tunaamini vijana wa Taifa Stars hawatakata tamaa ila watacheza kwa uwezo wao wote kuhakikisha wanapata matokeo yatakayoiwezesha timu kuvuka hatua hiyo muhimu katika safari hiyo ya kuelekea Morocco.
Tunatarajia wachezaji wa Stars watalipigania taifa kwa hali na mali, kuweka ubinafsi kando na kuwa kitu kimoja kuhakikisha wanapata matokeo yanayotakiwa ili timu isonge mbele.
Katikia mchezo wa kwanza tuliona udhaifu wa wachezaji kupoteza umakini uwanjani na hivyo kuigharimu Taifa Stars. Wachezaji wanatakiwa kufahamu wajibu walionao katika timu ya taifa.
Tunasema hivyo kwa sababu tunafahamu kazi ya mchezaji wa timu ya taifa ni kupigania kitu ambacho huwa na thamani na kumbukumbu kubwa kwa vizazi vingi vitakavyofuatia.
Kitu wanachotakiwa kuleta wachezaji wa timu ya taifa ni ushindi. Siku zote wachezaji wa timu ya taifa wanaposhinda huwa wanaliletea taifa lao furaha na kujisikia fahari kuishi katika taifa hilo, hivyo tunatarajia wachezaji wa Taifa Stars wanaelewa wana jukumu kubwa la kutuletea furaha wananchi wa Tanzania na kutengeneza historia zao kwa kuanzia mechi hii ya marudiano dhidi ya Msumbiji.
Tunatarajia uongozi wa timu pamoja na uongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF) wanakuwa karibu na wachezaji ili kuwatia nguvu na kuwapa kile ambacho kitaonekana ni muhimu kwa mchezo huo.
Itakuwa ajabu basi kusikia lawama zikitupiwa kwa watu tofauti kama timu itafanya vibaya, hiyo itamaanisha mtu fulani hakutimiza wajibu wake fulani kwenye timu na hivyo kusababisha matokeo mabaya.
Tunatarajia kutosikia hayo na badala yake kusikia lugha moja hata kama matokeo hayatakuwa mazuri au pale tutakapopata matokeo mazuri.
Vilevile tunatarajia kuona TFF, wadhamini, mashabiki pamoja na serikali wakiendelea kumpa ushirikiano mzuri kocha Mart Noiij ili aweze kuwandaa vizuri wachezaji wa Taifa Stars ili kuhakikisha ushindi unapatikana katika mechi ya marudiano dhidi ya Msumbiji.
Tunaelewa Taifa Stars ina kibarua kigumu, lakini pia tunaamini tuna wachezaji wazuri na wenye uwezo mkubwa kuliko wachezaji wa Msumbiji hivyo hatutakiwi kukata tamaa ya ushindi mwishoni mwa wiki.

Post a Comment

 
Top