LIGI Kuu Italia imenasa kitu kimoja kwenye fainali za Kombe la Dunia za mwaka huu zilizofanyika nchini Brazil.
Teknolojia ya waamuzi kutumia vinyunyizo
vinavyotoweka kwa haraka ili kutambua eneo lilipofanyika faulo na mahali
ambapo wachezaji wanapaswa kujipanga kuweka ulinzi.
Waamuzi wote kwenye fainali za Kombe la Dunia la
Brazil walitumia teknolojia hiyo. Kutokana na kuvutiwa na jambo hilo,
Ligi Kuu Italia (Serie A) na Ligi Daraja la Kwanza (Serie B) zimeamua
kuiga teknolojia hiyo na kwamba wataitumia kwenye ligi yao msimu ujao.
Hata hivyo, wakati Serie A ikijinadi kuiba
teknolojia hiyo kutoka kwenye Kombe la Dunia, mikikimikiki hiyo itatibua
hali ya mambo kwenye ligi hiyo kwa msimu ujao kutokana na nyota wake
wengi waliong’ara nchini Brazil kutakiwa na timu za ng’ambo na hivyo
huenda wasiwepo kwenye Serie A tena.
Jambo kama hilo limekuwa likitokea mara kwa mara
kila inapofanyika michuano mikubwa kwamba kwa wachezaji waliong’ara
wanaweza kuhama kutoka timu moja kwenda nyingine, lakini kwa Italia
ambayo klabu zake zinataka kujipanga ili kurejea makali yao kwenye Ligi
ya Mabingwa Ulaya, kitendo cha kuondokewa na wakali wake ni pigo.
Ligi Kuu Hispania ilitamba kwenye Ligi ya Mabingwa
Ulaya msimu uliopita kwa sababu klabu zake zinavutia wachezaji makini.
Jambo hilo ni sawa na Ujerumani.
Kwa misimu kadhaa iliyopita, Ligi Kuu England
ilikuwa ikitesa kabla kukumbwa na tatizo la kuondokewa kwa wakali wake
na hivyo klabu za nchi hiyo kuanza kukumbana na wakati mgumu kwenye
michuano ya Ulaya.
Sasa zinajipanga kujiweka sawa kwa ajili ya msimu
ujao huku Serie A ikiwa kwenye hatari zaidi kutokana na wachezaji wake
nyota ambao wanafanya ligi ya nchi hiyo kuwa na mvuto kuwindwa na timu
za nje.
Mauricio Isla
Kwenye umri wa miaka 26, Isla alionyesha kiwango
kikubwa kwenye Kombe la Dunia akiwa na kikosi cha Chile. Klabu yake ya
Juventus inaonekana kama haimtaki, lakini ukweli mchezaji huyo si wa
kuachwa aondoke kirahisi.
Juventus haimtendei haki kwa sababu tangu
alipojiunga na timu hiyo mwaka 2012, Isla hakucheza mechi nyingi na hilo
linamfanya staa huyo wa zamani wa Udinese kufikiria kuitema Serie A na
kwenda kusaka ulaji kwingine.
Isla ni mpambaji wa kweli ndani ya uwanja.
Anakimbia bila kuchoka na ni jambo la kawaida anapocheza kwa dakika
tisini kuona anakimbia zaidi ya Kilomita 11. Kwa mujibu wa Fifa, faida
ya kuwa na Isla kikosini ni kwamba anasaidia kwenye ulinzi na
kushambulia.
Alikuwa nguzo imara kwenye mtindo wa soka la kushambulia
uliokuwa ukitumiwa na Chile kwenye fainali za Kombe la Dunia. Pia ni
mchezaji ambaye makocha wamekuwa wakiwatumia kwa maelekezo maalumu ndani
ya uwanja. Alitumwa kumtuliza Neymar, akatulia.
Paul Pogba
Juventus inataka kuibakiza silaha yao hiyo makini,
lakini kwa kiwango kilichoonyeshwa na kinda huyo wa Kifaransa kwenye
fainali za Kombe la Dunia na kwenye Serie A msimu uliopita, ni wakati tu
haujafika kumshuhudia nyota huyo kwenye jezi za timu nyingine.
Timu nyingi zinamtolea macho Pogba. Lakini,
kuondoka kwake ni pigo kwa ligi ya Italia, kwa sababu ni wazi linapokuja
suala la kutaja mastaa wa ligi hiyo, Pogba ni miongoni mwa majina hayo.
Akiwa na umri wa miaka 21 tu, tayari Pogba
anatazamwa kama moja ya viungo makini zaidi duniani. Klabu za Chelsea,
Liverpool, Manchester City, Manchester United na Paris Saint-Germain
zote zinafukuzia saini ya staa huyo.
Jose Mourinho wa Chelsea ameripotiwa kutenga Pauni
60 milioni kwa ajili ya kumng’oa Ufaransa huyo kwenye Serie A na
kumrudisha kwenye Ligi Kuu England.
Juan Cuadrado
Kulikuwa hakuna wasiwasi wowote wa kwamba Juan
Cuadrado angeweza kuihama Fiorentina, lakini baada ya kiwango maridadi
alichokionyesha kwenye Kombe la Dunia nchini Brazil akiwa na kikosi cha
Colombia, wasiwasi sasa umekuwa mkubwa.
Kabla ya Kombe la Dunia alikuwa ni mchezaji
anayefahamika ndani ya Serie A pekee. Nje ya hapo hakukuwa na nchi
nyingine iliyokuwa ikimfahamu mchezaji huyo. Lakini, sasa amekuwa staa
mpya wa dunia na anazivutia timu nyingi.
Mchezaji mwenzake kwenye kikosi cha Colombia,
James Rodriguez ametesa sana kwa kuandikwa na magazeti. Si kama
hakustahili, isipokuwa kinda huyo wa AS Monaco alifaidika sana kwa
kucheza sambamba na Cuadrado kwenye fainali hizo za Brazil.
Cuadrado, hakika ndiye aliyeifanya Colombia kutesa
kwenye fainali hizo. Ni mchezaji mwepesi sana, ana kasi, mtaalamu wa
kukokota mipira na fundi wa kutengeneza nafasi za kufunga. Hilo lilikuwa
na faida kubwa kwa Rodriguez na hatimaye akafunga mabao sita na kuibuka
Mfungaji Bora kwenye fainali hizo.
Msimu uliopita alipangwa nafasi zote za pembeni.
Kuna wakati pia alitumika kama kiungo wa kati, kiungo mshambuliaji na
pia aliwahi kuchezeshwa kama straika. Cuadrado ni kiraka. Hivyo,
kuondoka kwenye Serie A ni pigo kubwa kwenye ligi hiyo.
Arturo Vidal
Kiungo wa Chile, Arturo Vidal, anatajwa kuwa
mchezaji bora duniani kwenye nafasi yake anayocheza. Kama atatangaza
kuhama klabu nyingi zitapigana kuinasa saini yake.
Vidal, 27, aliwasili kwenye fainali za Kombe la
Dunia nchini Brazil akiwa majeruhi, lakini alipona kwa haraka na
kuonyesha makali yake kwenye michuano hiyo.
Mwenyewe amesema atabainisha hatima yake ya msimu
ujao wakati atakaporejea Italia akitokea kwenye likizo baada ya
kumalizika kwa fainali za Kombe la Dunia.
Klabu ya Manchester United inamtaka na inaamini
atakuwa staa wao mpya katika kipindi cha wiki tatu zijazo japo kwamba
Liverpool nao wameingia vitani kwenye kumsaka nyota huyo.
Baada ya kuwa na pesa zilizotokana na mauzo ya
Luis Suarez aliyekwenda Barcelona, Liverpool sasa anajiona wana nguvu ya
kusajili kila mchezaji aliyepo mbele yao. Wanamtaka Vidal na Pogba.
Mario Balotelli
Mario Balotelli hakucheza vizuri sana kwenye
fainali za Kombe la Dunia zilizofanyika nchini Brazil. Hata hivyo,
kikosi cha Italia kwa ujumla hakikuwa kizuri wakati wa fainali hizo.
Balotelli alikwenda kwenye fainali hizo akiwa
kwenye presha kubwa. Hakufanya vizuri, lakini hilo halimzuii kuwindwa na
timu mbalimbali zinazohitaji saini yake.
Kabla ya fainali za Kombe la Dunia
straika huyo wa AC Milan alihusishwa na mpango wa kujiunga na Arsenal. Baadaye mambo yakagoma.
Aliporejea kutoka kwenye michuano hiyo miamba ya
soka ya Ufaransa, Paris Saint-Germain ilitajwa kuwania saini ya mchezaji
huyo huku Jose Mourinho na kikosi chake cha Chelsea akipiga hesabu kali
za kumnyakua.Kuondoka kwa Balotelli kwenye Ligi Kuu Italia ni pigo kwenye ligi hiyo
kutokana na ukweli kwamba mkali huyo ni moja ya nyota wanaolitambulisha
soka la nchi hiyo. Agosti kitakuwa kipindi kigumu sana kwenye Serie A
kutokana na klabu zake kuwa kwenye wakati mgumu wa kupambana kuwabakiza
nyota ili wasihame. Wengi wao walio kwenye hatari ya kuhama ni wale
waliotikisa kwenye fainali za Kombe la Dunia 2014 nchini Brazil.
Post a Comment