0
Morogoro. Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Morogoro, Dk Ritha Lyamuya amesema hali ya mtoto Devotha Malole aliyefichwa chini ya uvungu wa kitanda kwa miaka mitano inaimarika na kwamba bado anapatiwa matibabu.
Akizungumza jana, Dk Lyamuya alisema kwa sasa mtoto huyo anasumbuliwa na vidonda vilivyopo kwenye makalio vilivyosababishwa na kulazwa chini kwa muda mrefu pamoja na utapiamlo.
Alisema madaktari na wauguzi wamekuwa wakifuatilia kwa karibu afya ya mtoto huyo ambaye yupo kwenye chumba cha uangalizi wa karibu (ICU).
Dk Lyamuya alisema pamoja na matibabu mtoto huyo bado anaendelea kupatiwa lishe ili kurudisha afya yake iliyosababishwa na kukosa chakula bora kwa muda mrefu.
Dk Lyamuya alimshukuru Mbunge wa Jimbo la Morogoro Mjini, Abdulaziz Abood na Mkurugenzi wa Kampuni ya Alsaid, Omary Alsaid kwa kuwa tayari kumsaidia mtoto huyo .
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Leonard Paul alisema polisi wanaendelea na uchunguzi na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi kukamilika.

Post a Comment

 
Top