“Unakuta kwenye vyama tunazalisha tani 445 za korosho halafu unapata
sulphur tani 22 badala ya tani 100. Hii ndiyo sababu ulanguzi upo
kutokana na pembejeo kidogo zinazoletwa na Serikali. Kama pembejeo za
ruzuku zingekuwa zinatosha tusingekuwa tunalia na mfuko wa pembejeo,”
anasema Mchola.PICHA|MAKTABA
“Wakulima wa korosho tunaweza kuboresha uchumi wetu kama Serikali itakuwa na nia madhubuti ya kukuza na kuwekeza katika kilimo.”
Hayo ni maneno ya mkulima wa korosho wilayani
Tandahimba, Chiboko Ally (65). Anasema kuwa kama mkulima akiwekeza
kwenye kilimo na kuungwa mkono na Serikali, lazima uchumi utakua.
Kwa mujibu wa Ally, ni vigumu kwa mkoa kama Mtwara
kupata maendeleo ya kiuchumi kwa kutumia ardhi kwa kutegemea zao la
korosho licha ya kuwa ndiyo zao tegemezi kwa wananchi wake kwani mara
nyingi pembejeo zimekuwa zikicheleweshwa.
Hata hivyo, yapata wiki moja tangu mfuko wa
kuendeleza zao la korosho nchini (CIDTF), kuzindua rasmi ugawaji na
usambazaji wa pembejeo za ruzuku kwa msimu wa mwaka 2014/ 2015, kumekuwa
na malalamiko kutoka kwa wakulima wakisema ugawaji wa pembejeo umekuwa
kitendawili kutokana na upatikanaji wake kuwa mgumu.
Mkulima huyo anasema kuwa amekuwa akitegemea zaidi
pembejeo za ruzuku kutokana na bei yake kuwa na nafuu licha ya kuwa
hazikidhi mahitaji ya mkulima na kwamba wamekuwa wakiumia zaidi hasa
linapokuja suala la upuliziaji na maandalizi ya shamba.
Anaeleza kuwa amekuwa akijikita kwenye kilimo
hicho kwa miaka mingi hata kabla ya kuanzishwa kwa mfuko wa kuendeleza
zao la korosho nchini ambao unahusu zaidi ruzuku. malengo ya mfuko huo
yalikuwa ni kufanya mabadiliko kwa mkulima ili aweze kupata pembejeo za
kutosha na pia kuvuna kwa mafanikio.
“Nimezaliwa katika familia inayojihusisha na
kilimo cha korosho na kukulia katika zao hili kabla hata ya kuanzishwa
kwa mfuko huu wa pembejeo, lakini bado haujaleta mabadiliko ya
kuridhisha kwa mkulima licha ya kuwa na malengo mazuri,” anasema
Chiboko.
“Wito kwa Serikali ni kwamba iongeze zaidi
pembejeo ikiwezekana kutoa zaidi ya mara moja kwa msimu mmoja kwani kwa
sasa mfuko hutoa mara moja tu kwa msimu.”
Uhaba wa pembejeo
Kwa upande wake, Mlela Mlela ambaye ni mkulima wa
zao hilo, anasema mfuko wa pembejeo za ruzuku haujavutia, kwani mawakala
wanaosambaza pembejeo hizo wamekuwa wakiwapelekea wakulima kiasi
kisichotosha na kujikuta wakiwa kwenye wakati mgumu pindi wanapofanya
maandalizi ya kupulizia mikorosho.
Anaeleza kuwa unaweza kukuta mkulima anamiliki
shamba la ekari 20 halafu anapatiwa mifuko 10 ya pembejeo. Hiyo haikidhi
haja, hivyo kuwalazimu kununua nyingine kutoka kwa matajiri ambao
huwauzia kwa bei ya juu hali ambayo inazidi kuwadidimiza kiuchumi.
“Pembejeo hazikidhi mahitaji ya mkulima hata kidogo. Unakuta
mkulima una shamba la ekari 20, lakini unapatiwa mifuko 10 ambayo
haikidhi mahitaji na kutulazimu kununua nyongeza toka kwa machuuzi ambao
hutuuzia kwa bei ya Sh25,000 hadi Sh30,000 kwa mfuko wa kilo 25 tofauti
na zile za ruzuku ambazo kwa mfuko wa kilo 25 bei yake inakuwa
Sh15,000” anaeleza Mlela.
“Hali hiyo imekuwa ikizidi kutudidimiza wakulima
kiasi kwamba malengo yetu ya mwanzoni mwa msimu, hayatimii ikitokea hali
hiyo na kusababisha tuishie pabaya,” anasema Mlela.
Naye Arab Mchola, mkulima ambaye pia ni mwenyekiti
wa Chama cha Msingi cha Ushirika (Amcos) anasema kuwa kiasi kidogo cha
pembejeo wanachopatiwa wakulima, hakifanani na hali halisi na hivyo
husababisha kuwe na ulanguzi kutokana na mahitaji ya Serikali kuwa
madogo.
“Unakuta kwenye vyama tunazalisha tani 445 za
korosho halafu unapata sulphur tani 22 badala ya tani 100. Hii ndiyo
sababu ulanguzi upo kutokana na pembejeo kidogo zinazoletwa na Serikali.
Kama pembejeo za ruzuku zingekuwa zinatosha tusingekuwa tunalia na
mfuko wa pembejeo,” anasema Mchola.
Muda wa ugawaji wa pembejeo
Hata hivyo, malalamiko ya wakulima hao kutopata
pembejeo kwa wakati, ilimfanya mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Joseph Simbakalia
kuagiza wapatiwe pembejeo kwa wakati unaotakiwa.
Aidha, Yusuph Ally, mkulima wa korosho kutoka
Wilaya ya Tandahimba, anasema kuwa Serikali inatakiwa kuwasaidia
wakulima wapate pembejeo kwa wakati ili kupata mazao mazuri na kupunguza
umaskini kwani ndilo zao pekee linalotegemewa na wananchi walio wengi.
“Kuchelewa kwa pembejeo kunaathiri upatikanaji
mzuri wa mazao kwani inatakiwa wakati wa upuliziaji mkulima awe na
pembejeo za kutosha, lakini kwa hili limekuwa tofauti, licha ya kuwa
korosho ndiyo zao linalotegemewa zaidi hasa katika mkoa huu,” anasema
Ally
Kwa upande wake Katibu Mtendaji Mfuko wa
Kuendeleza Zao la Korosho nchini, (CIDTF), Suleiman Lenga, akizungumza
wakati wa ufunguzi wa pembejeo za ruzuku msimu wa mwaka 2014/ 2015,
anasema kuwa majukumu ya mfuko huo ni kuendeleza kilimo cha korosho kwa
kusaidiana na Bodi ya Korosho na pia umekuwa ukigharamia mafunzo ya
wakulima na waghani kwa ajili ya utafiti na dawa.
Lakini, Lenga anasema ugawaji wa pembejeo umeanza
hata kabla ya ufunguzi na kwamba msimu wa mwaka 2013/2014 haukufungwa na
kuwataka wakulima kulipa kiasi cha Sh15,000 kwa mfuko wa kilo 25 ili
kumpunguzia mkulima gharama za uzalishaji na kwamba pembejeo zipo za
kutosha.
“Lengo la Serikali ni kumpunguzia mkulima gharama
za uzalishaji kwani pembejeo zipo za kutosha hivyo mawakala wahakikishe
pembejeo zinamfikia mkulima kwa wakati na kwa gharama iliyopangwa na
hivyo wakulima wasikubali kununua pembejeo isiyo ya ruzuku,” anasema
Lenga.
“Pembejeo za ruzuku hutolewa kwa wakulima kulingana na mahitaji
kutoka kwa maafisa kilimo wa ngazi ya wilaya ambayo nao huyapata kutoka
kwa wagani wa kata ambao huzigawa kwa mujibu wa fedha zilizopatikana
kutokana na bajeti ya Serikali kupitia Wizara ya Kilimo.
“Hatuwezi kusema kwamba pembejeo za ruzuku ni
chache kwani huwa tunapokea mahitaji ya wakulima kupitia kwa maofisa
kilimo wa wilaya husika. Ndani yake kuna maofisa ugani kutoka katika
kata na pembejeo huwa tunazigawa kwa mujibu wa pesa tulizopata kwa
mujibu wa bajeti iliyopo ambayo hutolewa na Serikali,” anasema Lenga.
Hata hivyo, ofisi yake imekuwa ikiishauri Wizara
ya Kilimo kuongeza bajeti ya ununuzi wa pembejeo hizo za kilimo cha zao
la korosho ili kuinua zao hilo hapa nchini.
“Tumeiomba Serikali kuongeza bajeti ya pembejeo
ili kuweza kuwafikia wakulima wengi zaidi ili tufikie malengo yetu ya
kimkakati tuliyojiwekea” anasema Lenga.
Hata hivyo, baadhi ya wananchi wanawalalamikia
watu wanaohusika na pembejeo kwamba baadhi yao wamekuwa wakinufaika na
pembejeo kwa kuuza kwa bei ya juu.
“Tunaishauri Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na
Rushwa (Takukuru) kutoka makao makuu kupitia namna pembejeo zinavyouzwa
hovyo hapa Mtwara. Wananchi wengi hatutendewi haki, hali ni mbaya sana,”
anasema mmoja wa wakulima ambaye hakupenda jina lake liandikwe gazetini
kwa sababu za kiusalama
Post a Comment