Hamza Kalala,
Kuna wanamuziki ambao wamejipatia umaarufu mkubwa kupitia tasnia ya muziki, kwa kuufanya uvutie ndani na nje ya nchi.
Vile vile wanamuziki hao wamedumu kwenye tasnia
hiyo kwa zaidi ya miaka 40, miongoni mwa wanamuziki hao ni pamoja na
Hamza Kalala, ambaye amewahi kupewa majina kadhaa kama vile mzee wa
Madongo na Komandoo.
Historia ya Kalala kwa ufupi
Alizaliwa mkoani Tanga na kusoma shule za msingi na sekondari mkoani humo.
Baba yake Komando alikuwa mfanyakazi wa Shirika la
Reli, katika Stesheni ya Mpanda, ambaye baadaye alihamishiwa mkoani
Tanga ambako alibahatika kuoa mke wa kabila la Kizigua, ambaye ndiye
mama wa Komando Kalala.
Mara baada ya Komando kuzaliwa alipewa jina la ‘Kapesula,’ akiwa ni mchanganyiko ‘chotara’ wa makabila ya Kinyamwezi na Kizigua.
Komando Kalala alianza kuhamasika katika mambo ya
muziki mwaka 1966 akiwa darasa la nne, wakati alipokuwa akimshuhudia
baba yake akiimba na kucheza ngoma ya Kinyamwezi ya ‘Manyanga’ ambayo
ilitokana na ngoma ya ‘Hiyari ya Moyo’, huko huko Tanga.
Wakati huo wakata mkonge walikuwa wakifanya
mashindano ya ngoma kati ya Wanyamwezi na ngoma za makabila mengine
waliokuwa katika mashamba tofauti ya mkonge ya Kibaranga, Amboni na
mengine mengi.
Lakini ngoma ya ‘Manyanga’ ya Wanyamwezi na ile ya
‘Sindimba’ ya Wamakonde ndizo zilizokuwa zikitia fora katika mashindano
hayo kila mara. Kalala anaeleza, hakufundishwa muziki na mtu bali ni
kutokana na ngoma hizo alizokuwa akicheza na kuimba baba yake, na
kumuiga kupiga gitaa mjomba wake ambaye alikuwa na gitaa nyumbani.
Anasema alipima uwezo wake wa muziki alipokuwa
kwenye bendi zilizokuwapo kwenye mashamba ya Mkonge kama Kwanduru Jazz
Band, na Amboni Jazz.
Hakuvutiwa na maisha ya mashambani hivyo alirudi
Tanga Mjini, ambako aliendelea na mazoezi ya kupiga gitaa nyumbani kwao,
siku moja alipita Mkongo mmoja aliyekuwa akijulikana kwa jina moja la
Chivosha, akavutiwa kwa jinsi alivyokuwa akipiga gitaa na kumuomba
ajiunge na bendi yao ya Villa Negro Successes.
Anasimulia huku kote alikuwa anatoroka na baba
yake hakuwahi kufahamu kama anaimba, alichelea kumwambia kwa kuogopa
kukatishwa tamaa.
Anaeleza kuwa baba yake aliposikia kuwa mwanaye ni mwanamuziki
na anaimba na kupiga katika ukumbi wa Mwananchi, ulikuwa ukumbi maarufu
Mkoani Tanga, akaenda kumtafuta, lakini hakumtambua licha ya yeye
kumuona.
Kalala anasema, haikuwa rahisi kumfahamu kutokana
na alivyojiremba, kutokana na kuwapo katika bendi ya Wakongo ambao
wanapenda kujiremba.
Anasema wanawake wa viongozi wa bendi hiyo, kazi
yao kubwa ilikuwa ni kumremba, ambapo siku hiyo aliyokuja baba yake
alikuwa amechoma nywele, na alivaa nadhifu kama wanamuziki wa Kikongo
wanavyovaa.
“Moja ya sifa za mwanamuziki kufanya kazi na
wanamuziki wa Kikongo ilikuwa ni kuwa nadhifu, na wakiridhishwa na kazi
yako wapo radhi kukugharamia, wanawake wao walikuwa wanachukua karibu
nusu siku kunipendezesha, na kwa kweli nilikuwa nabadilika kabisa,
“anasema Kalala.
Anaendelea kueleza kabla ya kukutana na baba yake
ili kulitolea ufafanuzi suala hilo walipata safari ya Nairobi nchini
Kenya, akatoroka na aliporudi alimletea zawadi ya fulana ya kisasa
wakati huo, na kumueleza wazi kuwa alikuwa Nairobi, kimuziki na ndiyo
kazi anayofanya kwa wakati huo.
“Aliipenda sana zawadi niliyomletea, na alinisifia
kwa kujiheshimu kipindi chote kiasi cha yeye kushindwa kubaini kuwa
mimi ni mwanamuziki, na kunitaka niendelee kuwa na heshima katika kazi
yangu hiyo, “anasema Kalala.
Anasema anakumbuka fedha ya kwanza kulipwa katika
muziki ni Sh saba kwa mwezi ambayo yote aliimaliza kwa kununua nguo,
kama suruali pekosi, viatu raizoni na Itali vilivyokuwa vimechongoka
mbele kama mkuki, na mashati ya slimu fiti ambayo yalikuwa yanashika
mwili, ‘ukimkumbatia mtu limechanika’.
Anakumbuka jinsi alivyokuwa anapata taabu na kina
dada ambao walikuwa wanampapatikia kutokana na kuwa nadhifu, hadi kuna
kipindi alilazimika kujificha ili kuepuka usumbufu.
Anasema kifo cha bendi hiyo kilitokana na
kugombania fedha, kuna baadhi walisema hawalipwi vizuri, “ siku hiyo
walipigana sana, na walikuwa na miili mikubwa, sikuingilia ugomvi wao,
hivyo baada ya hapo bendi ilikufa kutokana na baadhi yao kuamua kurundi
kwao Kongo usiku huo huo.
Safari ya kwanza kutafuta bendi nje ya Tanga
Mwaka 1969, aliamua kumfuata mwanamuziki Abel
Bartazar ambaye alikuwa anaishi na kufanya kazi za muziki katika Mji
mdogo wa Kilosa Mkoani Morogoro, lakini kwa bahati mbaya hakumkuta.
Anasema aliamua kurudi Tanga kujipanga upya kabla
ya kuamua kwenda Moro kwa lengo la kutafuta kazi katika bendi za Moro
Jazz na Cuban Marimba.
Anasema hakuwa na ndugu wala jamaa Mkoani humo, hivyo
alilazimika kuuliza zilipo kumbi za starehe ambazo zilikuwa zinapiga
muziki wa dansi baada ya kushuka kituo cha mabasi.
Anaeleza kwa bahati mbaya akafahamishwa kuwa bendi
maarufu za muziki wakati huo Cuban Marimba na Moro Jazz, zilikuwa
ziarani mikoani ambapo Moro Jazz ilikuwa Zanzibar na Cuban Marimba
ilikuwa Songea, lakini kwa bahati nzuri alibakia mwanamuziki mmoja wa
Cuban Marimba, mpiga gitaa la solo anaitwa Waziri Nyange, akaelekezwa
alipo.
“Nilipofika nyumbani kwake alinipokea, nikajieleza
kuwa mimi ni mgeni nimetoka Tanga na nimekuja kwa ajili ya kutafuta
bendi ya kupigia muziki, akanikaribisha na kuniambia nitaishi kwake,
hadi bendi itakaporudi, ”anasema Kalala.
Kalala anasema, baada ya wiki moja bendi ya kwanza
kurudi ilikuwa ni Moro Jazz, hivyo akaenda kujieleza kwa Mbaraka
Mwishehe, ambaye alikuwa na taarifa ya uwapo wake, na kumkubali akanza
kupiga katika bendi hiyo.
Anasimulia aliporudi Juma Kilaza, kiongozi wa
Cuban Marimba hali ilikuwa tofauti, alimwita na kumueleza kwa nini
amejiunga na bendi hiyo wakati alipokelewa na mtu wao, kulingana na
ukweli alioambiwa ikabidi aondoke Moro na kujiunga na Cuban Marimba.
“Kilaza alikua mbabe kidogo, hivyo alikuja
kunichukua kwa nguvu Moro Jazz na mimi sikuwa na budi kukubali, kutokana
na ukweli walioniambia na hadi wakati huo nilikuwa naishi kwa Nyange,
”anasema Kalala.
Anaendelea kusimulia kuwa, licha ya kukubali
kujiunga na Cuban Marimba kutokana na hisani aliyofanyiwa na Nyange,
alikuwa anatamani sana kubaki Moro kutokana na ucheshi wa Mbaraka
Mwishehe na unadhifu waliokuwa nao wanamuziki wa Moro Jazz ukilinganisha
na Cuban Marimba.
Anasema kama kulikuwa na bendi zina upinzani wa
kweli wa muziki, ilikuwa ni hizi mbili, zilikuwa zinashindana na kupiga
muziki wa kweli, anazitaja nyimbo za majibizano zilizokuwa zinaonyesha
upinzani wao ni ule wa Moro Jazz, uliokuwa unaitwa ‘Moto wako washa nje
hapa maji yatazima’, na Cuban wakawa na mtindo kila baada ya kumaliza
wimbo wanasema ‘Dawa ya moto ni moto siyo maji’, ikiwa ni kama kuwajibu
Moro.
Anawataja wanamuziki aliowakuta Moro Jazz kuwa ni
pamoja na Mbaraka Mwishehe , Issa Khalfani aliyekuwa anatumia shoto na
alikuwa anapiga gitaa zote, Athumani Milingiti, Maneno, alikuwa anapiga
drums, Kokobile alikuwa mwimbaji, ambaye ndiyo aliyeimbiwa wimbo na
Baraka Mwishehe uitwao ‘kwa heri rafiki yangu mpenzi’, alipokuwa
anaondoka kwenda kwao Zaire.
Anayakumbuka mashairi ya wimbo huo kuwa ni ‘Kwa
heri, kwa heri rafiki yangu mpenzi, utapofika Zaire wasalimie mabingwa
wote wa muziki wa huko Zaire......Wasalime Franco na Ok Jazz’.
Anawataja wanamuziki waliokuwa wanaunda Cuban
Marimba wakati huo kuwa ni Juma Kilaza, mpiga solo Ufuta, Ally analikuwa
anapiga Rythm, mpiga bezi gitaa Juma Sangula, na mwimbaji Maselina.
Post a Comment