0
ar es Salaam. Kampuni ya Mantra Tanzania na Idara ya Wanyamapori ya Wizara ya Maliasili na Utalii (Wildlife Division) zimesaini mkataba wa makubaliano ambao umelenga pande mbili kushirikiana katika kupiga vita ujangili wa tembo katika eneo la Kusini mwa Hifadhi ya Wanyamapori ya Selous.
Katika makubaliano hayo, Kampuni ya Mantra Tanzania itawekeza Dola za Marekani 800,000 kwa mwaka 2014 katika kampeni dhidi ya ujangili nchini.
Makubaliano hayo yalisainiwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Uranium One Inc, Chris Sattler kwa niaba ya Mantra Tanzania, kampuni dada ya Uranium One inayosimamia Mradi wa Mto Mkuju, mgodi mkubwa duniani wa urani katika ukanda wa kusini wa nchi.
Akizungumzia hali ya ujangili nchini, ofisa mtendaji huyo alisema, “Ujangili wa ndovu umefikia hatua mbaya katika Hifadhi ya Wanyamapori ya Selous na Kampuni ya Mantra imejipanga kikamilifu kuchukua hatua madhubuti ili kukabiliana na tatizo hili,” alisema Sattler na kuongeza:
“Makubaliano haya yanaturuhusu kushirikiana na Idara ya Wanyamapori, kuandaa na kuutekeleza mpango wa kupiga vita ujangili ili kuwaokoa ndovu waliopo katika Hifadhi ya Selous. Napenda kumshukuru Waziri Nyalandu kwa uongozi wake katika suala hili la msingi. Najua wote tuna matumaini kuwa mpango huu utasaidia kuonyesha njia kwa kampuni binafsi na za umma kushirikiana katika kuhifadhi wanyamapori.”
Waziri Nyalandu alisema Serikali ya Tanzania ambayo inaunga mkono mradi huo, itahakikisha masuala mengine yaliyosalia yatasainiwa kabla ya Juni.

Post a Comment

 
Top