0
Okocha  

ATIKA dimba la Uwanja wa Taifa wa Ufaransa, maarufu kama Stade de France, Juni 28, 1998, Watanzania walikuwa wameganda katika luninga zao wakishindwa kuamini kuwa timu ya Afrika waliyokuwa wanaishabikia katika Kombe la Dunia ilikuwa imekufa kwa mabao 4-1 kutoka kwa Denmark.
Ndio, kama ilivyo kwa Waafrika wengine, Watanzania walikuwa wamejipa ushabiki wa timu ya Taifa ya Nigeria. Lakini Peter Moller akaipatia Denmark bao la kwanza. Brian Laudrup akaipatia bao la pili, Ebbe Sand akaipatia la tatu, Thomas Helveg akaipatia la nne. Dakika mbili baadaye, Tijani Babangida akaipatia Nigeria bao la kufutia machozi.
Kwanini Watanzania tulikuwa mashabiki wa Nigeria? Kwanza kabisa walikuwa wametukosha katika fainali za Kombe la Dunia mwaka 1994 nchini Marekani. Pili wakatukosha kwa kutwaa medali ya dhahabu ya Olimpiki pale Atlanta Georgia Marekani.
Hata baada ya kupigwa na Denmark Watanzania wakaendelea kuwa mashabiki wa Nigeria. Mpaka leo bado wapo mashabiki wa Nigeria nchini. Mashabiki wa damu. Lakini unadhani Wanigeria wana tofauti kubwa kisoka na sisi? Hapana.
Wanigeria wanajituma katika kuhaha kutafuta maisha. Taifa lao lina watu zaidi ya milioni 170 kwa sasa. Kila Mnigeria anajituma kadri anavyoweza. Huyu anatapeli, yule anacheza soka, huyu anaimba, mwingine anaanzisha dhehebu feki la dini. Ili mradi mkono uende mdomoni.
Na ni kwa njia hii ndio Wanigeria wametugeuza kuwa mashabiki wao. Vipaji vya wachezaji wao ni hivi hivi vya wachezaji wetu. Tofauti ni katika kutafuta maisha. Yakubu Aiyegbeni ndiye Edward Chumilla. Waliomwona Sunday Manara hawamtofautishi sana na Jay Jay Okocha.
Peter Rufai alikuwa kipa wa kawaida asiyefikia uwezo wa Mohamed Mwameja wala Riffat Said. Hata mabao manne waliyofungwa na Denmark alichangia kiasi kikubwa kufungisha.
Baada ya soka lao, Watanzania tulihamia katika filamu zao. Mama zetu, dada zetu na watoto zetu wakahamia katika kupenda filamu za Kinigeria. Ukweli ni kwamba hawakuwa na jipya sana ambalo sisi hatukuwa nalo.
Mastaa wao Nouah Ramsey, Desmond Elliot, John Okafor, Ini Edo na wengineo wana vipaji ambavyo Tanzania vilionekana tangu zama za akina Bishanga na wengineo. Tatizo ni uwezo wa Wanigeria kubuni vitu viwili vitatu kama vile kuingiza mambo mengi ya kishirikina ambayo tulikuja kuyaiga.
Hata hivyo maudhui yao ni yale yale ya kawaida ambayo wacheza filamu wetu wameyazoea. Mara nyingi unakuta mtoto wa tajiri amempenda masikini. Hakuna jipya sana, hakuna sehemu ambayo wanaweza kuangusha ndege kama Hollywood wanavyofanya na filamu zao za kusisimua.
Tatizo hapa wacheza filamu wetu hawajitumi. Wengi hawana vipaji wala elimu. Wanacheza filamu kwa sababu walikuwa Mamiss, wanamitindo au wamerudi kutoka katika Shindano la Big Brother. Vinginevyo hatuangalii vipaji. Tunaangalia wauza sura.
Matokeo yake tumejikuta tukirudi kuwa mashabiki wa Filamu za Kinigeria bila ya sababu za msingi. Hakuna unachoweza kufanya zaidi ya kucheka. Mcheza filamu yuko bize na matajiri kuliko kujikita katika kazi yake apate pesa za kuwa tajiri.
Hata hivyo kama vile haitoshi, baada ya Wanigeria kutuchukua kutoka katika soka na filamu, sasa wametuteka katika muziki. Nenda katika baa maarufu popote Tanzania, au nenda katika ukumbi maarufu wa disko ukasikie jinsi nyimbo za mwanamuziki Davido wa Nigeria zinavyotuteka.
Wimbo wake wa Aye kwa sasa ni kama wimbo wa taifa wa muziki. Kabla ya hapo wimbo wake wa Skelewu ulikuwa gumzo lililopitiliza. Lakini ukichunguza sana katika nyimbo zake, hakuna cha ajabu ambacho Watanzania hawawezi kufanya.
Wimbo wa Aye unamuonyesha akiwa shambani. Lakini kama Diamond Platinumz akipiga nyimbo inayomuonyesha akiwa mashambani watu watapuuza. Hata yeye mwenyewe hataki. Aliwahi kufanya wimbo mmoja akiwa kijijini, lakini haukuvuma.
Ndio maana sasa anafanya video za kifahari Afrika Kusini, anaonekana akirekodiwa kutoka angani na vifaa vya kisasa. Kwanini Davido anatuteka zaidi ya Diamond? Kwanza ni kwa sababu ya kupenda Unigeria ambao umetuingia.
Pili wenzetu wamefanikiwa kujitangaza kimataifa. Vipaji ni vilevile tu, lakini kama P Square wanafanya wimbo na Ricky Ross huku wewe unamtafuta Jackline Wolper na kujaribu kumfanya kuwa mwanamuziki ili auze sura katika wimbo wako wakati hana kipaji chochote cha muziki.
Muziki wanaoufanya Wanigeria tunaweza kuufanya. Mimi ni mmoja kati ya watu wanaoamini hilo. Tatizo ni wanamuziki wetu kukosa ubunifu, au Watanzania wenyewe kuwa wepesi katika mapokeo ya kila kitu.

Post a Comment

 
Top