0
Dar es Salaam. Pambano la bondia Francis Cheka la kuwania ubingwa wa dunia unaotambuliwa na Shirikisho la Ngumi za Dunia (WBF), sasa litafanyika Juni 6 kwenye Ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar es Salaam.
Cheka, ambaye awali alipangwa kuzichapa na Varely Brudov wa Urusi, amebadilishiwa mpinzani na sasa atazichapa na bondia kutoka Uingereza.
Akizungumzia pambano hilo, Cheka alisema tayari ameanza kambi ya wazi jijini Dar es Salaam kujiwinda na pambano hilo na kusisitiza kuwa lengo lake ni kuhakikisha anatwaa tena ubingwa huo aliovuliwa mwishoni mwa mwaka jana.
“Nategemea wiki ijayo kwenda Morogoro kujifua milimani kwa ajili ya kujenga pumzi, lakini pia natarajia kuweka kambi nje ya nchi kujiwinda na pambano hilo,” alisema Cheka.
Wakati huohuo, kocha mkuu wa timu ya taifa ya judo iliyoweka kambi nchini Uturuki kujiandaa na Michezo ya Jumuiya ya Madola, Hamis Zaid amesema kikosi chake hivi sasa kimekubaliwa kujifua na timu ya taifa ya nchi hiyo baada ya kuonekana kufikia viwango.
Zaid alisema awali walipowasili nchini humo hawakukubaliwa kuanza mazoezi na timu ya taifa kutokana na kiwango chao na kukabidhiwa timu ya vijana ya nchi hiyo kabla ya kufuzu hatua ya awali na kupewa nafasi ya kujifua na timu ya taifa ya nchi hiyo.
“Wenzetu wana programu ya muda mrefu ambayo hivi sasa tunajitahidi kwenda nayo pamoja na mwelekeo wetu hivi sasa ni mzuri.”
Kocha huyo aliyeambatana na wachezaji Andrew Thomas, Abubakar Nzinge na Mbarouk Selemani alisema programu hiyo itafanyika hadi Juni 29 ikiwa ni mwezi mmoja kabla ya kuanza kwa michezo hiyo.

Post a Comment

 
Top