0


Ujumbe wa Tanzania ukiangalia ramani ya Singapore inayoonyesha ujenzi wa miundombinu na makazi mbalimbali  ya watu. Picha na  Neville Meena. Meenaaktaba. 
Mnunuzi wa nyumba Singapore analipa aina moja ya kodi.
Singapore. Mambo haya matatu ni kikwazo cha kukua kwa sekta ya nyumba nchini na tunapozungumzia sekta hii hatuwezi kuweka kando Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) ambalo limeanza kujenga na kuwauzia Watanzania nyumba bora za kuishi.
 Mambo haya mosi, ni riba kubwa ya mikopo ya nyumba ya asilimia 18 inayowekwa na benki, pili ni kodi nyingi ambazo zinatozwa katika vifaa vya ujenzi na tatu ni bei kubwa ya ardhi kwa ajili ya ujenzi wa nyumba hasa maeneo ya mijini.
 Nchini Singapore baadhi ya wabunge walifanya ziara kujifunza jinsi nchi hiyo ilivyowekeza na kupata mafanikio katika sekta ya makazi. Somo la kujifunza asilimia 82 ya watu milioni 5.3 nchini humo wanaishi katika nyumba zao.
 Asilimia 18 iliyobaki sawa na watu 954,000 tu wanaishi katika nyumba zilizojengwa na sekta binafsi na wengine kati ya hao wanamiliki nyumba zao wenyewe.
 Dalili za umahiri wa kuendeleza makazi inaonekana tu unapoingia eneo la kukagulia hatia za kusafiria katika Uwanja wa Ndege wa Changi, kwani mbele kuna tangazo kubwa linalonadi utaalamu huo katika nchi hiyo ya Mashariki mwa Bara la Asia.
 Majengo na miundombinu mingine katika nchi hiyo ndogo yenye ukubwa wa kilometa za mraba 700,  yamepangiliwa kwa  ustadi wa hali ya juu.
 Wananchi hawajengi nyumba hizo wenyewe, bali ni kazi ya Serikali, ambayo licha ya kwamba inaendelea kukusanya fedha za mauzo mwaka hadi mwaka, imeweka utaratibu wa kusimamia kwa maana ya matunzo, matengenezo na kukusanya kodi ya majengo na ardhi.
Mpango wa matumizi ya ardhi ulioandaliwa 1971 na kuanza kutekelezwa miaka 16 baadaye, 1987.
Matumizi ya ardhi yanajumuisha barabara, reli, bandari, viwanja vya michezo, maduka, maeneo ya ukanda wa kijani, viwanda na sehemu nyingine nchini Singapore.
 Serikali ya Singapore ilitwaa ardhi karibu yote kwa sheria ya Bunge ya 1966 na kuiwekea malengo ambayo yameleta manufaa makubwa.
Shughuli za ujenzi na uendelezaji wa makazi zinafanywa na Kampuni ya Surbana inayomilikiwa na Serikali.
 Ofisa Mtendaji Mkuu wa Surbana, Profesa Louis Tay anasema Surbana hawanunui ardhi bali hupewa rasilimali hiyo kutoka katika Benki ya Ardhi ya Serikali na kutekeleza mradi unaohitajika.
 Katika mchakato wa ununuzi wa nyumba, benki za Singapore zinatoa mikopo ya muda mrefu kati ya miaka 15 na 20, kivutio kikubwa katika mikopo hiyo ni riba ambayo ni kati ya asilimia 2 na 3 tu, viwango ambavyo ukizidisha mara sita ndio unafikia viwango vya Tanzania.
 Kwa upande wa kodi, uongozi wa Halmashauri ya Mji wa Pwani ya Mashariki nchini Singapore, uliuambia ujumbe wa Tanzania kwamba mnunuzi wa nyumba hulipa kodi ya aina moja tu na kwa kuwa nyumba hizo ziko kwenye ghorofa moja, kodi husika hugawanywa kwa idadi ya wanunuzi hao, hivyo ina unafuu mkubwa.
Tanzania
Tukirejea Tanzania wapangaji wa NHC na waliouziwa nyumba, idadi yao ni sawa na asilimia 0.2 tu ya Watanzania wote na hii inamaanisha kwamba watu wanaoishi katika nyumba hizo hawafiki hata 100,000.
 Hivi sasa NHC wana wapangaji takriban 17,000 na  nyumba ambazo zimeuzwa kwa watu mbalimbali tangu 1961 ni 8,883, kati ya hizo 5,383 ziliuzwa tangu lilipoanzishwa na mwaka 2010 zaidi ya nyumba 500 zimeuzwa kati ya mwaka 2011 na sasa.
 Utafiti uliofanywa na Chuo Kikuu cha Ardhi 2012, ulibainisha kuwa wapangaji wa nyumba za NHC wako katika makundi matatu kwa kuzingatia idadi ya wanafamilia; asilimia 43.3 ya nyumba hizo zilikuwa na watu kati ya wanne na watano, asilimia 32.5 watu kati ya mmoja na watatu na asilimia 20 zilikuwa na idadi ya watu sita na kuendelea.
 Hii inamaanisha kwamba zaidi ya asilimia 99 ya Watanzania wanaishi ama katika nyumba za kupanga zilizojengwa na watu binafsi, nyumba za Serikali au nyumba zao wenyewe.
 Licha ya kwamba nchini Tanzania watu hutumia nguvu zao kujenga, Taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) inaonyesha kuwa nchi inakabiliwa na upungufu wa nyumba milioni 3, huku kukiwa na mahitaji mapya ya nyumba 200,000 kila mwaka.
 Kwa upande wa ardhi, Tanzania hakuna mpango kamili wa matumizi ya ardhi uliopitishwa na mamlaka rasmi. Hili ndilo chimbuko la la migogoro mingi ambayo imesababisha baadhi ya watu kupoteza maisha.
 Baadhi ya wabunge ambao walikuwa nchini Singapore katika ziara ya mafunzo kuhusu uendelezaji wa makazi, wanasema hasara ya kuwa na ardhi isiyopimwa ni kukosa mapato kutokana na kodi.
 Mbunge wa Kawe, Halima Mdee anasema hali hiyo pia ni kichocheo cha migogoro ya ardhi.Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Goodlucky Ole Medeye anasema: “Tatizo kubwa ni fedha, uwezo wa kupima ardhi tunao na tunaweza kufanya hivyo katika muda wa miaka mitano tukawa tumemaliza nchi nzima endapo fedha zitapatikana.”
Kodi ya makazi
Wengine wanalalamikia ukubwa wa gharama za nyumba za NHC ambao unachangiwa na Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).
 Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Andrew Chenge akizungumzia suala hilo anasema: “Katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara, ni Tanzania pekee ambayo inatoza kodi kwenye makazi, hili ni jambo la ajabu kabisa, aliyeishauri Serikali kuhusu suala hili aliwapotosha.

Post a Comment

 
Top