0
Osama bin Laden aliitikisa dunia, ingawa ni kwa kipindi kifupi tu. Kwa kutumia kundi lake la Al Qaida, Osama alihusishwa kwenye mashambulizi kadhaa mabaya sehemu mbalimbali duniani yaliyosababisha vifo vya watu. Kubwa kuliko yote ni lile lililotokea Septemba 11, 2001, nchini Marekani. Kutokana na hali hii Osama akawa mwanadamu anayesakwa kwa udi na uvumba. Jina lake likawa maarufu kupita kiasi na waandishi mbalimbali wakaandika makala, chambuzi na hata vitabu kumhusu. Kwenye simulizi hii iliyotafsiriwa kwa Kiswahili na MIKI TASSENI, tunapata mtiririko wa mambo jinsi yalivyopangwa na yalivyotokea hadi bin Laden alipokamatwa na kuuawa akiwa katika maficho nchini Pakistan.
Jana tuliona jinsi al Qaeda ilivyokuwa ikifanya mashambulio ‘ola’ na kusababisha vifo vingi vya Waislam, jambo ambalo lilimhuzunisha sana Sheikh…
“Hapa kuna jambo muhimu ambalo tunatakiwa kuliangalia: kufanya mashambulio kadhaa bila kuchukua tahadhari, ambako kumeathiri hisia za makundi ya watu katika Taifa kuhusu mujahidin. Itapelekea sisi kushinda mapambano kadhaa huku tunashindwa vita mwishoni.
“Inahitaji mpangilio mzuri wa kila shambulio kabla ya kulifanya, pia kupima faida na hasara zake, halafu kuamua ni shambulio gani linafaa zaidi kufanya,” anaelekeza bin Laden.
Hata mafanikio yalimsumbua. Wakati wa mzingiro wa Khobar, Saudi Arabia mwezi Mei 2004, kundi kubwa la magaidi lilichukua mateka kutoka visima viwili vya mafuta na kuua wageni 19. Washambuliaji hao walikuwa sehemu ya “Al Qaeda katika Ghuba ya Arabuni, tawi la Yemen. Walikuwa wamewauliza mateka hao kila mmoja kama walikuwa Waislamu, na kuchana makoo ya wale ambao hawakuwa Waislamu. Wengi kati ya watekaji hao waliuawa katika operesheni ya uokoaji, na tukio hilo lilisaidia kuanzisha kampeni katili ya serikali ya Saudia dhidi ya wafuasi wa siasa kali.
Sheikh sasa alikuwa anaonya dhidi ya kufanya mashambulio kama hayo na mengineyo katika nchi za Kiarabu.
“Utawala uliopo utachukua hatua kali dhidi ya mujahidin; hii itapelekea kujilinda wao wenyewe na kulipa kisasi kwa utawala,” aliandika. “Ndugu wapiganaji na utawala watakuwa sasa katika vita ambayo hatukuanzisha, kwa sababu nguvu ya ndugu wapiganaji haitoshi kwa vita kama hiyo.
“Mkakati unaofaa ni kukwepa mapambano na serikali za Kiarabu, kama Yemen, Iraq na Saudia, kukwepa kumaliza nguvu zetu katika kukabiliana na serikali hizo katika kipindi hiki (na) kupoteza hisia chanya za Waislamu kuhusu sisi. ..
Sisi ndiyo tunawalinda Waislamu na kupigana na adui yao mkubwa, umoja wa Makrusedi na Wazayuni.”
Ilikuwa inatosha sasa kuwa ‘watu kwa jumla’ wanaona kuwa wanaoathirika ni Waislamu, hata kama bin Laden, kwa viwango vyake vinavyochuja zaidi, alikuwa hakubali hivyo. Kuwaua wanaoingia katika kundi hilo, pamoja na kuweza kutetewa kimaadili, ilikuwa ni kosa la kimkakati. Bora mashambulio ya baadaye yaje kutoka maeneo mbali na Mashariki ya Kati, alisema. Alitaja Korea ya Kusini kama mfano.
“Kati ya nafasi za kutumia katika kuwalenga Wamarekani ni hali dhaifu ya usalama inayoonekana katika nchi ambazo hatujafanya mashambulio yoyote.”
Sheikh mara nyingi alikuwa anafundisha katika barua zake, akijaribu kuuelekeza mtandao wake kuelekea katika malengo yake makuu. Alikuwa na wasiwasi siyo tu kuwa matawi rasmi ya Al Qaeda yalikuwa yanaambaa mbali na uelekezi wake, lakini malengo yake yalikuwa yanavurugwa kwa kulenga vitu na mahitaji ambayo aliyaona hayana umuhimu.

Post a Comment

 
Top