0
Tume ya Mabadiliko ya Katiba juzi ilizindua rasimu ya Katiba Mpya iliyopendekeza mambo mengi ikiwa ni pamoja na Uhuru wa habari na vyombo vya habari inayovitaka kusambaza habari kwa kuzingatia utu, heshima na staha.
Rasimu hiyo inaeleza kuwa kila mtu anao uhuru wa kutafuta, kupata na kutumia habari na taarifa na kusambaza taarifa hizo.
Inafafanua kwamba masharti ya Ibara hiyo yatalazimika kuzingatia masharti ya sheria ya nchi itakayotungwa kwa ajili hiyo na kwa madhumuni ya kulinda usalama wa taifa, amani, maadili ya umma, haki, staha na uhuru wa watu wengine.
“Kuanzisha vyombo vya habari na njia nyingine za upashanaji wa habari bila kujali mipaka ya nchi, vyombo vya habari vitakuwa huru na vilevile vitakuwa na haki ya kupata, kutumia na kusambaza habari na taarifa” inaeleza rasimu hiyo.
Inafafanua kwamba vyombo vya habari vitakuwa na wajibu wa kusambaza habari na taarifa kwa wananchi na kuheshimu na kulinda utu, heshima, uhuru na staha ya wananchi dhidi ya habari na taarifa wanazozitumia, wanazozitayarisha na kuzisambaza.
Inaeleza kuwa Serikali na taasisi zake, asasi za kiraia na watu binafsi watakuwa na wajibu wa kutoa habari kwa umma juu ya shughuli na utekelezaji wa shughuli zao. kufuatia hali hiyo baadhi ya wadau wa habari wamesema rasimu ya katiba hiyo inaonyesha mwelekeo mzuri wa utendaji kazi za habari nchini.
Wamesema kila nchi vyombo vya habari vyake vinafanya kazi kwa kuzingatia masharti ya sheria inayolinda masuala ya usalama wa taifa . Kwa kuzingatia hayo wamesema kinachotakiwa ni kuwapo kwa uhuru wa vyombo vya habari.

Post a Comment

 
Top