0


 
 


Posted  Jumanne,Juni5  2013  saa 22:26 PM
Kwa ufupi
Hakuna anayeweza kupinga ukweli kwamba kupatikana kwa Katiba mpya ya Tanganyika ni jambo la lazima kabla ya mwisho wa mwaka ujao, ili Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano ikianza kutumika mwaka 2015 Watanganyika nao wawe tayari wamepata Katiba yao

Baada ya Tume ya Marekebisho ya Katiba juzi kuandika historia kwa kutoa rasimu ya awali ya Katiba mpya kwa kupendekeza mabadiliko makubwa ya kimfumo na uendeshaji wa nchi yetu kwa siku zijazo, hatua hiyo sasa imetengeneza ombwe upande wa Tanzania Bara, kwa maana ya Watanganyika nao kuhitaji Katiba mpya kabla ya mwaka 2015.
Wazanzibari wanayo Katiba yao ya mwaka 1984 ambayo ilifanyiwa marekebisho mwaka 2010. Hivyo, tunaweza kusema pasipo shaka kwamba mabadiliko ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano hayatailazimisha Zanzibar kuandika Katiba mpya, ingawa inaweza kufanya marekebisho ya hapa na pale katika Katiba hiyo ya 1984 kwa lengo la kukidhi matakwa mbalimbali yatakayotokana na Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano.
Hakuna anayeweza kupinga ukweli kwamba kupatikana kwa Katiba mpya ya Tanganyika ni jambo la lazima kabla ya mwisho wa mwaka ujao, ili Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano ikianza kutumika mwaka 2015 Watanganyika nao wawe tayari wamepata Katiba yao. Ni bahati mbaya kwamba mchakato wa kupata Katiba mpya ya Serikali ya Muungano haukuwa umepangwa, bali ulianza ghafla kutokana na shinikizo la vyama vya upinzani na asasi za kiraia.
Kwa maneno mengine, iwapo suala la kupata Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano lingekuwa limepangwa na kupata mwafaka wa kitaifa mapema, mchakato wa kupata Katiba hiyo nao ungeanza mapema angalao mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010. Kutokana na hali hiyo, mchakato huo ulikuja kama jambo la dharura na ndiyo maana Tume ya Warioba ililazimika kufanya kazi usiku na mchana kukusanya maoni ya wananchi, kuyaratibu na kutoa rasimu ya awali ya Katiba mpya katika muda mfupi.
Kwa kukubali shinikizo la vyama vya upinzani na vuguvugu la mageuzi la kutaka ipatikane Katiba mpya kabla ya mwaka 2015, Rais Jakaya Kikwete alionyesha busara, uzalendo na ujasiri wa hali ya juu kwa sababu aliiepusha nchi yetu isiingie katika machafuko ya kisiasa. Sote tulikuwa mashahidi wa jinsi viongozi wengi wa chama chake, wakiwamo wabunge walivyokakamaa wakipinga kuandikwa kwa Katiba mpya, huku baadhi wakitaka Katiba ya sasa iwekwe viraka tu.
Hivyo, ieleweke kwamba kuchelewa kuanza kwa mchakato wa kupata Katiba mpya ya Muungano halikuwa tatizo la Rais Kikwete. Ndani ya CCM ilikuwamo minyukano na mikikimikiki iliyotokana na mifarakano ya kiitikadi na kisera ya muda mrefu, kwani wahafidhina hawakutaka Katiba mpya kwa hofu ya kupoteza dola. Ni kwa sababu hiyo Rais alionekana kusimama peke yake akitafuta mwafaka wa kitaifa kwa kukutana na kupokea mapendekezo ya upinzani na asasi za kiraia kuhusu Rasimu ya Sheria ya Marekebisho ya Katiba ambayo ingejadiliwa na kupitishwa na Bunge, hivyo kuruhusu mchakato wa Katiba mpya kuanza.
Tumesafiri mwendo mrefu na kupita kwenye milima na mabonde na kuweza kufika hapa tulipo. Sasa tunayo Rasimu nzuri ya awali ya Katiba Mpya. Wakati mchakato huo ukiendelea, tungependa kumshauri Rais Kikwete azindue mchakato mwingine wa kupata Katiba ya Tanganyika ili ipatikane hata kabla ya Katiba ya Muungano. Rais amefanya kazi nzuri mpaka sasa. Na huo ndiyo utakuwa urithi wake kwa Watanzania atakapomaliza kipindi chake cha kuiongoza nchi yetu mwaka 2015.


.

Post a Comment

 
Top