0
New York, Marekani. Tanzania imesisitiza kuwa ushirikiano wa kimaendeleo ni eneo muhimu katika kupunguza umaskini na katika kuzijengea uwezo na mazingira ambayo hatimaye yataziwezesha nchi zinazoendelea kupunguza utegemezi.
Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Fedha Mwigulu Nchemba kwenye mjadala kuhusu hatua za kimataifa kuelekea 2015 na mifumo ya ufuatiliaji na uwajibikaji kwa ushirikiano wa kimaendeleo.
Nchemba ambaye alikuwa mmoja wa wanajopo wanne walioongoza mjadala huo uliohusisha mawaziri, wabunge, wasomi, wafafiti na wajumbe kutoka Taasisi zisizo za kiserikali duniani, alisema uanzishwaji mpya wa ushirikiano wa maendeleo baada ya mwaka 2015, unatakiwa kuendelezwa kama ulivyoainishwa katika lengo la nane la Malengo ya Milenia (MDGs).
Mkutano huo ambao hufanyika kila baada ya miaka miwili umefanyika chini ya mwamvuli wa Baraza la Umoja wa Mataifa linalohusika na Masuala ya Uchumi na Maendeleo ya Jamii (ECOSOC).
Akitilia mkazo kuhusu eneo hilo la ushirikiano wa kimaendeleo, Naibu Waziri alisema ushirikiano huo lazima pia ujengeke katika mazingira ya kuaminiana, kuwajibika na kuwa na mifumo ya ufuatiliaji.
Akizungumzia kuhusu misaada ya maendeleo (ODA), kuwa ingawa misaada hiyo ya maendeleo bado ni muhimu hususan kwa nchi zinazoendelea, lakini mchango wake si mkubwa sana katika eneo la maendeleo kwa ujumla wake. Nchemba aliyataja maeneo ambayo yanaweza kuzalisha mapato mapya ya ndani kuwa ni pamoja na ukusanyaji wa kodi na udhibiti wa fedha chafu.
“Uimarishaji wa vyanzo hivyo vya mapato, udhibiti wake, uwajibikaji pamoja na ushirikiano wa kimaendeleo, ndipo mataifa yanayoendelea yataweza kupunguza utegemezi wa misaada kutoka nje,” alisisitiza Nchemba.

Post a Comment

 
Top