Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh
Dodoma. Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG)
atatumia siku 45 kuchunguza kashfa ya ufisadi wa zaidi ya Sh200 bilioni
zilizolipwa kwa Kampuni ya Kufua Umeme ya IPTL kutoka katika Akaunti ya
Escrow.
Habari za uhakika zilizolifikia gazeti hili jana,
zinasema CAG amemwandikia barua Katibu wa Bunge, akimwomba athibitishe
rasimu ya hadidu za rejea 13 ambazo zitamwongoza katika ukaguzi huo
unaosubiriwa na Bunge, wanasiasa na wananchi.
Moja ya hadidu za rejea ni uchunguzi wa iwapo
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) aliisamehe kampuni hiyo kodi
inayofikia Sh26 bilioni.
Mwishoni mwa wiki, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda
alilieleza Bunge kuwa ukaguzi katika akaunti hiyo ungefanywa na Ofisi ya
CAG na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
Sakata la hilo la IPTL liliibuliwa na Gazeti dada
la The Citizen na Mwananchi, baadaye Mbunge wa Kigoma Kusini, David
Kafulila (NCCR-Mageuzi), akalipua bungeni ufisadi katika Akaunti hiyo ya
Escrow iliyofunguliwa katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT).
Akichangia Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu wiki
iliyopita, Kafulila aliliomba Bunge liunde kamati teule kuchunguza
ufisadi huo akisema ni mkubwa kuliko ule Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA)
ambayo pia ilikuwa ya BoT.
Hoja yake iliungwa mkono na wabunge kadhaa
akiwamo, John Mnyika (Chadema - Ubungo), ambaye alipinga Takukuru
kuchunguza akisema ndiyo iliyoisafisha Serikali katika kashfa ya
Richmond.
Hata hivyo, baada ya mvutano mkali, Spika wa
Bunge, Anne Makinda alitumia mamlaka yake kukubaliana na pendekezo la
Waziri Mkuu la kutaka CAG na Takukuru wachunguze.
AG Frederick Werema alipopigiwa simu jana kuhusu suala hilo alisema: “Nimepumzika, sina muda wa kujibu maswali yako.”
Barua ya CAG
“Pamoja na barua hii, ninaleta rasimu ya hadidu za
rejea zilizounganishwa na zile zilizotoka kwa Katibu Mkuu Nishati kwa
ajili ya kuridhiwa na ofisi yako kabla ya ukaguzi maalumu kuanza,”
inasomeka sehemu ya barua hiyo ambao CAG Ludovick Utouh alikiri
kuiandika akisema: “Ni kweli nimewatumia hizo hadidu za rejea.”
Kuhusu muda wa uchunguzi, Utouh alisema: “Hizo
siku 45 ni makadirio tu lakini tutafanya kwa sababu tunajua kuna
shinikizo kubwa linahusika ila itategemeana pia na ugumu wa kazi
tutakayokutana nayo.”
Mkurugenzi wa Shughuli za Bunge, John Joel alipoulizwa jana
alisema ingawa hajaiona, amesikia kuwapo kwa barua hiyo katika Ofisi ya
Katibu wa Bunge.
Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah ambaye ofisi yake ilipokea barua hiyo Aprili 23, mwaka huu, hakupatikana jana.
Maeneo yatakayozingatiwa katika ukaguzi huo
yametajwa kuwa ni pamoja na CAG kuchunguza utekelezaji wa mkataba wa
kuzalisha umeme kati ya IPTL na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).
Kuchunguza iwapo BoT ilitimiza wajibu wake na
kuchukua tahadhari ya kutosha kabla ya kuhamisha Dola 22,198,544.60 za
Marekani na Sh8, 020,522,330.37.
Pia, CAG ametakiwa kuchunguza iwapo BoT ilitimiza
wajibu wake na kuchukua tahadhari wakati wa kuhamisha hati fungani zenye
thamani ya Sh153.36 bilioni kutoka Escrow kwenda IPTL.
Katika hadidu hizo za rejea, CAG anatakiwa
kuchunguza sababu za kufunguliwa kwa Akaunti ya Escrow pia chanzo cha
mgogoro kuhusu tozo kati ya Tanesco na IPTL.
Kwa mujibu wa barua hiyo ambayo gazeti hili
limeiona, CAG atachunguza iwapo wakati akaunti hiyo inafunguliwa,
Kampuni ya Mechmar ilikuwa ina hisa za umiliki katika Kampuni ya IPTL.
“Pia kuthibitisha kama Mechmar ilikuwa imehamisha
umiliki wake kwenda Kampuni ya Pan African Power Solution (PAP) kabla ya
kufilisiwa,” inasomeka moja ya hadidu za rejea.
Kulingana na hadidu hizo za rejea, CAG pia
anatakiwa kuchunguza kiwango cha fedha kilichopaswa kuwapo kwenye
Akaunti ya Escrow wakati BoT inahamisha fedha kwenda IPTL.
Kazi hiyo ya CAG itahusisha pia kuchunguza na
kutoa taarifa kuhusu kiasi cha fedha kilichowekwa na kila mhusika hadi
uamuzi wa Mahakama Kuu kuhusu kesi ulipotolewa.
“Kuchunguza madai ya Benki ya Standard Chartered
(Hongkong) kwa IPTL na madai mengine ya kuzalisha umeme wa IPTL na kama
Serikali imejihadhari na uwezekano wa madai yanayoweza kufunguliwa dhidi
yake na wadai mbalimbali,” inasomeka barua hiyo ikiomba Bunge
lithibitishe hadidu hizo kabla ya kuanza ukaguzi.
Pia CAG atachunguza iwapo Wizara ya Nishati na
Madini ambayo iliingia mkataba na IPTL kufungua akaunti hiyo ilifanya
uadilifu na kuweka uangalifu kabla ya kutoa fedha zilizokuwapo kwenye
akaunti.
CAG amegizwa pia kufanya uchunguzi kuhusu hisa za Mechmar
inayosemekana kufilisika na iliyokuwa na hisa nyingi IPTL na kama hisa
hizo sasa zinamilikiwa na PAP na ametakiwa kutoa mapendekezo ya njia
sahihi za kisheria zinazoweza kutumika kwa ajili ya kulinda Serikali
isipate hasara katika utekelezaji mkataba wa IPTL.
Ukaguzi huo utahusisha pia shughuli zote
(transaction) zilizofanyika kuhusiana na suala hilo kuanzia Julai Mosi,
2006 hadi Machi 31, mwaka huu na wakaguzi wameruhusiwa kuongezea
mawanda.
Post a Comment