0
Arusha. Jaji Mkuu nchini, Mohamed Chande Othman, amevitaka vyombo vya dola, viongozi na wananchi kufanya kazi kwa kuheshimu Katiba na Utawala wa Sheria badala ya kujichukulia sheria mkononi.
Akizungumzia suala la utii wa sheria nchini, mara baada ya kufungua kongamano la kwanza la majaji wanawake barani Afrika, alisema kila mtu yupo sawa mbele ya sheria.
“Lazima ieleweke nchi hii inaongozwa kwa kufuata misingi ya sheria, hairuhusiwi mtu yeyote kutumia mamlaka yake kukiuka sheria kwani kila mtu lazima aheshimiwe , haki haitegemei uzito wa mtu au pesa ya mtu” alisema Jaji Chande.
Alisema Serikali inapaswa kuheshimu sheria, polisi wanapaswa kuheshimu sheria na pia raia wanawapaswa kuheshimu sheria hata kama zina upungufu.
“Kama sheria ina upungufu inafaa kupelekwa bungeni katika chombo cha kutunga sheria na sio kuvunja sheria,” alisema Jaji Chande.
Alisema katika kufuata misingi ya sheria na utawala bora kila chombo katika jamii kina nafasi yake.
“Polisi kazi yao ni kuchunguza, Idara ya Mwendesha Mashtaka ni kushtaki na Mahakama ni kutoa hukumu “alisema Jaji Chande.
Alisema ni lazima mwamko wa kuheshimu sheria uwepo na kuepuka watu kujichukulia sheria mikononi kama kujiita watu wenye hasira kali.
“Kila mtu anapaswa kuheshimu na kutii sheria na hakuna ambaye yupo juu ya sheria”alisema Jaji Chande.
Kauli ya Jaji Chande imekuja siku moja baada ya kuibuka sakata la kushambuliwa kwa kinachodaiwa ni risasi, Katibu wa Taasisi ya Kutetea Haki za Waislam nchini, Sheikh Ponda Issa Ponda. Tukio hilo la aina yake, lililotokea mkoani Morogoro, wakati Sheikh Ponda akiwa anaelekea kuswali katika msikiti wa Mungu Mmoja Dini Moja, baada ya kumalizika mhadhara katika Kiwanja cha Shule ya Msingi Uwanja wa Ndege.
Sheikh Ponda alilazwa hospitali ya Taifa Muhimbili kwa matibabu , lakini Serikali imepewa jukumu la kuhakikisha inafanya kazi ya ziada kutoa maelezo yaliyo sahihi juu ya tukio hilo.
Polisi wametangaza kuunda tume kuchunguza tukio hilo na wameahidi kushirikiana na vyombo vingine. . dola.

Post a Comment

 
Top