Kuna semi maarufu za wahenga kuwa, ‘Usipoziba ufa utajenga ukuta’ na ‘Heri ya nusu shari kuliko shari kamili’.
Semi hizi na nyinginezo zimekuwa zikitolewa kwa
lengo la kutoa hadhari kuwa ni muhimu kuchukua hadhari kabla ya kupatwa
na janga.
Tunaambiwa kuwa usipoziba ufa utajenga ukuta
tukipewa angalizo kuwa tusipozuia tatizo kabla halijawa kubwa, kwkazi ya
kulitatua itakuwa ngumu kwa kusubiri hadi liwe kubwa, kiasi kwamba
litashindikana kabisa kutatuliwa.
Katika jamii yetu tuna biashara ambazo zimekuwa
zikifanywa zikiwamo za kuuza fedha au chenji ambazo zinaonekana kwa
wingi katika mitaa yetu ikiwamo kwenye vituo vya mabasi.
Biashara hii siyo ngeni machoni mwa watu wengi kwani karibu kwenye kila kituo cha basi jijini Dar es Salaam inafanyika.
Biashara hii hufanyika baina ya makondakta wa daladala na wauza chenji kwa kutoa noti na kupewa sarafu.
Kwa kiasi fulani, biashara hii nayo ni moja ya
zile zilizopunguza uhaba wa ajira kwa vijana baada ya vijana kujiajiri
bila kujali ni wa umri au kabila gani, ingawa wengi wanaofanya biashara
hiyo ni vijana ambao wako tayari kukimbizana na magari katika baadhi ya
maeneo.
Katika baadhi ya maeneo biashara hii inafanywa na
watu wa rika zote kwa kuwa hukaa na fedha ambazo wamezipanga kwenye meza
na wateja wakija hununua tena kwa utulivu.
Ni biashara ambayo imetoa ajira, imepunguza adha,
ugomvi baina ya makondakta na abiria wao, imepunguza hata uhalifu kwa
kuwa vijana wengine ambao wangefanya mambo hayo sasa wamepata kazi ya
kufanya vizuri zaidi kwani wamejiajiri.
Hata hivyo, wasiwasi wangu ni kuhusu vijana wanaofanya biashara hiyo kutokujua madhara kwa afya na kutokufahamu athari zake.
Wataalamu wa afya na tafiti mbalimbali zinaonyesha
kuwa fedha hasa sarafu zina madhara kwa afya ya binadamu kutokana na
mzunguko wake ulivyo mkubwa.
Kwa mfano, tunaambiwa kuwa fedha inatembea kuliko pengine anavyotembea mtumiaji wake.
Haichagui wa kuitumia, wanaitumia wenye akili timamu na hata
wasiokuwa nazo, hivyo inategemea mtu wa mwisho aliitumia vipi kwa kuwa
kuna watu wanajifutia jasho noti bila kujali kuwa atampa mtu mwingine.
Kuna baadhi ya watu wanahifadhi fedha hizo zikiwamo sarafu na noti kwenye sehemu zisizo salama.
Tunaambiwa fedha zina madhara, wakati mwingine
zinaweza kusababisha maradhi kwa kuwa zinabeba vimelea vya magonjwa kwa
urahisi kutokana na kuwa katika mzunguko siku zote.
Uchunguzi umebaini kuwa fedha za noti na zile za
sarafu huweza kukusanya na kusambaza vimelea vya magonjwa hatari kutoka
kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine.
Vimelea hivyo vina uwezo wa kusababisha maradhi
kama ya ngozi, kuharisha, magonjwa ya fizi, homa za vipindi na
mengineyo. Kibaya zaidi magonjwa mengi huchukua muda hadi kujitokeza na
yanapojitokeza huwa tayari yameshaleta madhara ambayo yameingia mwilini
taratibu bila mhusika kujua.
Pamoja na kubeba vimelea hivyo, lakini fedha pia
inao uwezo wa kubeba sumu kutoka eneo moja kupeleka lingine kulingana na
mzunguko wake.
Kwa hiyo, ushauri wangu kwa wauza chenji na wateja
wao ambao kazi yao kubwa ni kushika fedha baadhi wamekuwa wakijisahau
na kula huku wakiwa nazo mkononi. Wanashauriwa waache tabia hiyo.
Post a Comment